Monday, March 18, 2013

JITAMBUE, JIPANGE ILI UFANIKIWE


                                                     SURA YA KWANZA:
    Anza kujipanga:
    Ili upate mafanikio siku zote unahitaji shauku ya dhati katika kufanikisha hilo sanjali na mkakati wa vitendo. Kuwa na shauku ya dhati itakusaidia kufanya mambo yako kwa vitendo zaidi, sababu vitendo ndiyo mafanikio yenyewe, ukizingatia hili mafanikio yatakuja kama ambavyo wewe unataka. Lakini je, ni kweli una hamu ya mafanikio katika maisha yako? Ndo swali la kujiuliza, kama jibu ndiyo, je, mipango yako ipo wapi?  Unataka kufanikiwa nini katika maisha? Na kwa vipi utafanikiwa? Unafanya nini ili kupata hayo mafanikio?  Je, upo tayari kubadili mfumo wa maisha yako? Upo tayari kuyafuatilia malengo yako? Na je, upo tayari kutathimini malengo yako mara kwa mara? Hayo ni maswali mengine unayopaswa kujiuliza pia.  

Kuishi maisha ya mafanikio ina maana ni hali unayokuwa umeitafuta, inaweza kukuchukua miaka kuifikia au kukamilisha malengo yako kama tu utaendelea kuweka hai ndoto zako za mafanikio. Fomula ya mafanikio ni rahisi lakini unashindwa kufanikiwa sababu hauna shauku ya dhati ya kutaka kufanikiwa au hauna mkakati madhubuti kufikia malengo hayo. Kwani kama unataka kufaulu mtihani ni lazima usome kwa bidii, na kama unataka kuwa na afya njema ni lazima ufanye mazoezisana.                                                                                                                                                                   

Hilo ndilo unalotakiwa kufanya hata unaposaka mafanikio, lazima ufanye jitihada ili kufikia mafanikio hayo. Na pia ili ufanikiwe unahitaji kujifunza mbinu mpya za mafanikio, hakuna jinsi kwa sababu hakuna njia ya mkato katika hili.
Kama unaifanyia kazi shauku yako ya kutaka kufanikiwa na unakuwa na mkakati madhubuti, ni wazi mafanikio utayaona na yatakuja kama ulivyopanga.
Ni muhimu kujifunza kupitia uzoefu wako katika maisha kwani maisha ndiyo mwalimu mkubwa wa kukuongoza. Kila hatua unayopitia katika kusaka mafanikio inakupa wazo jipya, na kama hupati wazo jipya basi tambua kwamba unapitia hatua zisizofaa.  
Siku zote mafanikio yanachochewa na mawazo mapya unayoyapata katika kila hatua unayopitia unaposaka mafanikio.

Watu wengi hujifunza kupitia maisha, kwani busara ndiyo hutumika kupambana na vikwazo vinavyojitokeza katika harakati za kusaka mafanikio.
Pia ni muhimu sana kuyafanyia kazi mawazo mapya unayoyapata katika kila hatua unayopiga kwenye kusaka mafanikio.
Endelea kuyafanyia kazi mawazo hayo kila mara kwa kuwa bila kufanya hivyo unaweza kupoteza malengo yako.
Mafanikio siyo ushirikina lakini unaweza kujikuta unaingia huko kusaka mafanikio, kama hauna mikakati ya kweli kwa ajili ya mafanikio. 

Jipange kufikia mafanikio ambayo tayari unayo ila tu hujui namna ya kuyapata.
Kila mtu amefanikiwa ila namna ya kuyaona mafanikio hayo ndiyo inayomsumbua kila mmoja wetu. Na kama utatulia ukajipanga vyema huku ukipangilia malengo yako ni wazi mafanikio utayaona bila tatizo lolote, kwani waliofanikiwa walikuwa kama wewe tu. Kwahiyo anza sasa kuyasaka mafanikio kwa nguvu zote hujachelewa bado.

Njia kubwa ya kupata mafanikio katika maisha ni kujua namna ya kutumia vyema mawazo, akili yako na upeo wako wa kufikiri katika kusaka mafanikio.
Upeo wako wa kufikiri ndiyo unaozalisha mawazo ambayo hukusaidia katika kufanikisha mambo mbalimbali unayoyahitaji katika maisha.
Ingawa kuna wakati unaacha kufanyia kazi mambo mema na kuruhusu yasiyo mema kutawala mawazo yako na kugeuza mambo ya kweli katika maisha yako ya kila siku.
Akili yako ni kama kiwanda cha kuzalisha yale yote unayoyataka.
Ni jukumu lako kuhakikisha unatawala na kutumia ipasavyo akili, mawazo na upeo wako wa kufikiri kwa ujumla katika kusaka mafanikio.

Kama kweli utaweza kutumia akili yako, ni wazi utashangaa  namna ambavyo mafanikio yatakavyokuwa yanakuja kwa urahisi kwako bila hata kutumia njia zisizo sahihi.
Kuwa na matarajio ya dhati katika yale mambo ya msingi, kwani hayo ndiyo mambo unayotakiwa kuyafikiria katika akili yako huku ukijenga picha halisi ya jambo unalolifikiria.
Kwa kufanya hivyo utaona fursa nyingi zinajitokeza mbele yako na kwa kuwa utakuwa na matarajio nazo hautakuwa na muda wa kupoteza katika kuzitumia fursa hizo.

Watu wengi huwa na mawazo ya kufanikisha ndoto zao na kutamani ndoto hizo kuwa kweli kwa muda mfupi, jambo hili linawezekana ingawa si kwa muda mfupi kama wengi wanavyotaka. Chukua muda kufanyia kazi mawazo yako, vinginevyo utakuwa mtu wa kufikiria vitu tu bila kuvifanyia kazi.
Kitu ambacho unaweza kukiongoza katika maisha yako ni kile unachokiingiza katika akili yako pamoja na mawazo uliyonayo akilini mwako.
Akili yako inafanya kazi jinsi unavyoiongoza, kama utaiongoza katika uoga hivyo ndivyo itakavyofanya kazi pia.

Lakini kama una mawazo mema na yenye mtazamo wa mafanikio basi hauko mbali na malengo na ndoto zako, hii ni kwasababu tu unaongoza vyema mawazo yako.
Na kama unajua unachokitaka lakini ukaruhusu mawazo mabaya yatawale akili yako basi tambua kwamba hautafanikiwa.
Kujua unachokitaka  na kujua kufikiria, ina maana mafaniko kwako yatakuja kama ulivyopanga na mwanga utauona katika maisha yako. 

Jitahidi kuyaepuka mawazo mabaya, kaa mbali na watu ambao wanaweza kuchangia mawazo mabaya  ambayo yatakuondolea mawazo ya kimafanikio.
Fikiria mawazo mapya, jua unachokitaka , tazama mafanikio yako yanafananaje, tafuta mawazo yatakayokufanya uwe katika muongozo wa mafanikio.
Suala hili linahitaji moyo na mtazamo wa kweli kufanya mawazo mazuri kuwa tabia yako na mfumo wa maisha yako.
Siri ya kufanikiwa katika maisha yako ni kufikiria mafanikio tu, mbali na hilo mawazo mazuri yatakufanya uwe na uchaguzi mzuri katika mambo yako utakayoyafanya kwa ajili ya mafanikio.



Mafanikio hutokea pindi unapokuwa umejikita katika malengo na ndoto zako na kuhakikisha ndoto na malengo vinatimia.
Mtu anayesaka mafnikio hachoki kufanya kazi kwa sababu haoni kama anafanya kazi, hii sababu  anaipenda kazi yake  au anapenda anachofanya au anafanya anachopenda.
Siri nyingine ya kupata mafanikio ni kuwa muwazi kila mara ili uweze kupambana na changamoto mpya, kwa sababu hauko sahihi wakati wote, inamaana utakuwa unajifunza kila mara. Mafanikio unayo ndani ya mawazo yako, kumbuka kama utashindwa kutumia uwezo wa akili na mawazo mazuri uliyobarikiwa na muumba basi ni wazi mafanikio kwako hayatapatikana katika hali uliyoitarajia.

Mafanikio hayaji bila kufanya kazi kwa bidii, na ili ufanikiwe unahitaji kuwa na malengo, si rahisi kuwa na mafanikio katika maisha kama huna malengo, kwani ni rahisi sana kuwa na mafanikio kama una malengo.  
Ili uweze kufanikiwa katika maisha ni lazima uamini kuwa unaweza kufanikiwa, bila ya kuwa na imani hiyo huwezi kufanikiwa kwa kuwa tayari hutakuwa na ari ya kufanikiwa.  
Mafanikio hayaji kwa siku moja ni lazima uyatafute kwa kufanya kazi kwa bidii na nidhamu, bila vitu hivyo ni vigumu kufanikiwa. 

Unaweza kufanya kazi kwa bidii kila siku katika maisha yako lakini bila ya kuwa na nidhamu na kile unachokipata katika kazi zako huwezi kufanikiwa, ili uweze kufikia malengo yako ni muhimu kudhibiti na kutumia kwa uangalifu chochote unachokipata katika shughuli zako.
Pia ni lazima uwe mtu ambaye unatambua kuwa wewe ni nani katika dunia hii na maisha yako kwa ujumla. Kwa kufanya hivyo utakuwa unajua unahitaji nini katika maisha yako, lazima pia uzingatie ulikotoka kwani maisha yako ya awali yana mafundisho mengi sana ambayo ukiyatumia kujfunza itakusaidia kupata mafanikio yako binafsi.

Baadhi ya watu huogopa kukumbana na changamoto lakini ni muhimu kufahamu kuwa katika maisha kushindwa au kukutana na changamoto zozote zile ni kama kuiona fursa nyingine mbele yako. Kama utakuwa unatumia changamoto hizo kujifunza vitu vipya kila siku basi itakusaidia kwa kiasi kikubwa katika harakati zako za kutafuta mafanikio.
Wengi wanaogopa kushindwa au kukutana na mitihani kwa sababu wanahisi itawaumiza mioyo yao, na pengine hata kuivunja kabisa.

Lazima tufahamu kuwa hata dunia huwa na majira yake ambayo huleta mabadiliko katika maisha yetu, na mabadiliko hayo huwa tunakabiliana nayo katika hali yoyote ile ambayo majira hayo yatakuja nayo.
Vivyo hivyo na hali ya kushindwa au kukutana na changamoto, vitu hivyo viko katika maisha yetu ya kila siku na yanaweza kuja katika hali tofauti kulingana na wakati.
Ni wajibu wa kila mmoja kuhakikisha anachukulia kushindwa kwake au kuzitumia changamoto anazokutana nazo katika njia zake za kuelekea kwenye mafanikio kuwa ni fursa mpya zinazojitokeza na hana budi kuzikubali na kuzitumia kupata mafanikio.
 Wengi hatujui ni nini kilichomo katika maisha yetu, na ili kujua tulichojaaliwa ndipo hapo suala la kushindwa au kukutana na changamoto huwa tunaliweka kando.


Maumivu ya kushindwa tunayoyapata huchangia katika kutuhamasisha tusikate tamaa ila tuendelee kutafuta kile tulichojaaliwa ndani yetu na kuweza kukitumia kupata mafanikio.
Bila kushindwa au kukutana na changamoto, hatuwezi kuwa na moyo wa kufanya jambo lolote la kimaendeleo na kutimiza ndoto zetu za kupata mafanikio.
Chukulia changamoto kuwa ni mwanzo wa kitu kipya na ambacho ni bora zaidi, na usichukulie changamoto kama ndio mwisho wa safari yako ya mafanikio.
Unaweza kupata chochote katika maisha kama tu una nia ya kutumia fursa zilizopo kupata hicho unachokihitaji.

Ndoto yoyote inayotawala mawazo yako huishia kuwa kweli, na mwishowe utapata matokeo mazuri. Hebu fikiria juu ya watu waliopata mafanikio, unafikiri walilala wakaamka na kuwa na mafanikio waliyonayo leo, hapana walihangaika na kukutana na vikwazo tele.
Kwanza walikuwa na mitazamo chanya juu ya kile walichokuwa wakikiota na kukiwaza siku zote, ni nadra sana kumkuta mtu aleyefanikiwa akisema siwezi au jambo hilo gumu sana kulifanya. Lakini  angalia watu wasio na mafanikio mara kwa mara huongea katika hali ya kukata tamaa na maneno yao huwa siwezi au jambo hilo ni gumu kulifanya.
Lakini ni uchaguzi wako, chochote unachokifanya kinaamuliwa na mawazo yako, la
msingi ni kujipanga na siyo kulaumu watu, hii ni kwa ajili ya mustakabali wako.

Siri ya kuwa mwenye nguvu katika jamii ni moja tu, nayo ni kufanya vitu kwa nguvu, usahii na umakini mkubwa ili wengine wakuamini bila kukutilia mashaka yoyote.
Tatizo kubwa ni kwamba miongoni mwa wengi ni kutaka kuwa na nguvu bila kutenda mambo kwa usahii. Tufahamu kuwa ukitaka kuwa na ushawishi lazima watu wakuamini, ili wakupende unatakiwa kuishi kwa wema, ili uwe na marafiki inabidi uwavutie kwa tabia zako uwe mwana jamii wa kujitolea, ujuzi utafute kwa kusoma na kujifunza kila siku, mafanikio yatafute kwa kujishughulisha kwa bidii sana bila kuchoka.
Jamii ikikuamini kwa matendo yako utakuwa na nguvu tu.

Siku zote kumbuka kwamba ili upate unachokihitaji inabidi kwanza uamue kukipata. 
Na tena ni lazima ujue ni nini haswa unataka, ndipo na akili yako itajua unataka nini.
Pia ni vizuri kuandika kwenye karatasi ili iwe rahisi kwako kukumbuka, kwani kila kitu kipo akilini na hapo ndipo kila kitu huanzia. Unapojua kile unachokihitaji hiyo ndio hatua ya kwanza katika kukipata.
Tambua ya kwamba unaposhindwa kupanga basi unapanga kushindwa kila kitu.
Usiogope kujaribu kwani binadamu kazaliwa ili afanye makosa, kwa kuwa nguvu mbili za mema na maovu ndani ya mwili wake zinashindana, hivyo ataendelea kusumbuka mpaka pale nguvu moja itakapomshinda mwenzake ndipo ushindi upatikana.


Jinsi wenzetu wanavyotuathiri katika maisha yetu

Hakuna binadamu aliyezaliwa Malaya, jambazi, mwizi nk. Wote kwa namna zetu tumekuwa tulivyo kwa sababu ya harakati za maisha.
Pengine litakuwa swali la msingi kujiuliza kwanini kusiwepo na aina moja tu ya binadamu, tofauti na tuonavyo leo ikiwa wote tumezaliwa wasafi?
Je, kati yetu wapo waliopenda kuwa vile walivyo [yaani wahalifu,  Malaya, wavuta madawa nk.] ? Tafiti hazioneshi kwamba wahalifu walichagua tabia hiyo, wengi kati yao hawakumbuki ni lini ilikuwa siku yao ya kwanza kujitumbukiza kwenye tabia hizo chafu.
Kama hilo halitoshi miongoni mwa watu waliofungwa  na tamaa za ngono walifanyiwa utafiti walionesha kutojua mwanzo wa tabia zao na kufanya kuwe na jambo la kujiuliza tena, kwanini hawajui na iweje wasikumbuke vitu walivyochagua kuvifanya katika maisha yao?

Katika hali ya kawaida umalaya ni nembo{utambulisho wa mtu/ kitu} kama watengeneza bidhaa wanavyofanya wanapozalisha mali zao.
Ili mtu ajue kwamba ile ni bidhaa Fulani lazima mtengenezaji achukue jukumu la kuiweka jina na kuibandika ili kumuwezesha mtu kuitambua.
Hata mungu katika uumbaji wake alivitambulisha vitu kwa nembo kama tunavyoviita leo. Hebu tujiulize tena ni nani aliyewawekea nembo majambazi, makahaba nk. tunaowaona leo mpaka jamii ikafikia hatua ya majina hayo? Hapa kuna haja ya kujifunza zaidi.

Siku zote waweka nembo ni watengenezaji bidhaa, hivyo wakiwepo majambazi, wezi na makahaba miongoni mwetu hawakufika hapo kwa hiyari yao bali walitengenezwa na binadamu wenzao, ambapo utafiti unaonesha kuwa watu tunaowaamini na kuwapenda sana ndiyo wenye nafasi kubwa ya kutubandika nembo mawazo na tabia zao.
Katika hali ya kawaida kila binadamu ana mtazamo wake, lakini wengi kati yao hawajiamini katika mienendo yao na hivyo kuwa tayari kusikiliza na kufuata mitazamo ya wengine bila kulinganisha na kuhakiki ukweli.

Wengi wetu tulikuwa watu safi kwa sababu tulikuwa na mtazamo wa aina hiyo.
Lakini kwa mshangao tukajikuta nasi tunaingia taratibu kwenye tabia za marafiki zetu tukaanza kuiba, kunywa pombe na mambo yafananayo na hayo.
Tunaweza kujiuliza kwanini tumefikia uamuzi huo? Jibu ni kwamba tumekubali binadamu wenzetu watupige nembo za uhuni, ujambazi, ukahaba, ushilikina nk.
Tumekubali kuwaunga mkono wenzetu walioshindwa kujenga ambao wanatuambia  kuwa kwa maisha ya leo ni vigumu kujenga kwa mshahara mdogo tunaolipwa, na sisi kwa kutokuwa na uwezo wa kupambanua tunakata tamaa kabisa ya kujiwekea malengo ya kujenga.

Hivi ndivyo binadamu wenzetu wanavyotufanya tuishi kwa mtazamo na mawazo yao,
tunabadili mitazamo yetu kwa kuiga fikra zao, tunajisikia vibaya kwa tafsiri zao na wakati mwingine tunaona aibu kwa sababu ya wenzetu wanavyotusema na kutupachika majina ya hovyo.  Kifupi hivyo ndivyo wanavyotuwekea nembo wenzetu ambao ni marafiki zetu, ndugu na jamaa zetu tena wakuaminiwa sana.   

Uchunguzi unaonesha kwamba asilimia 98 ya binadamu wanaishi kwa msukumo kutoka kwa watu wengine, lakini jambo baya zaidi ambalo linaweza kuwa la msingi kufahamu ni kwamba asilimia 89 kati ya hao wanaoathiriwa na wenzao kwa kupigwa chapa mbaya huku asilimia 11 tu ndiyo ikitajwa kufanikiwa kwa kufuata mambo mema yafanywayo na wengine. Labda tujiulize kwanini wengi wetu huathirika kwa sababu ya mitazamo ya wengine na nini cha kufanya? Jibu ni kwamba tumekuli kuacha kujiamini na kuanza kuishi kwa hofu ya kile wanachotafsiri wenzetu kuhusu sisi.
Siku zote uwezo ni kitu cha ndani, sasa inakuaje mtu mwingine atuambie kuwa hatuna uwezo na sisi tumwamini na kunyongea kwa lebo yake?

Una miaka kumi kazini lakini hata kiwanja huna, hujaanza kujenga unaogopa ukishindwa watu watakucheka. Unaacha kusoma kwa sababu kuna mtu/watu wanakuambia hauwezi kufaulu, unakuwa mtumwa wa mapenzi kwa kumng’ang’ania mpenzi asiyekutaka kwa kuwa unaogopa akikuacha huwezi kumpata mwingine.  
Kamwe usikubali kupigwa lebo na mtu mwingine, simamia  imani yako na misimamo yako. Iga mafanikio ya wengine na si kushindwa kwao kiasi cha kujikuta umekuwa mwizi/jambazi au changudoa/kahaba sababu ya kumfuata rafiki asiye na dira katika maisha. Hebu tuache kukubaliana na mitazamo ya wengine kuhusu maisha yetu.
Tuwapuuze wanaotuita majina mabaya, tukatae kufuata mkumbo na tusikubali kuona aibu kwa mitazamo ya marafiki zetu wa karibu. Maisha ni sisi tukiweza au tukishindwa wa kuwajibika ni sisi wenyewe.

Kama unataka kufanya kitu kisicho cha kawaida ni lazima pia ukubali na matatizo yasiyo ya kawaida, na ufurahie kuyakabili kwani ni shart la maisha.
Pamoja  na hayo ili kuwa salama tunatakiwa kuwa chini ya uangalizi wa kitu/mtu mwingine yaani jamii, utamaduni au mazingira yanayotuzunguka.
Kuna mambo lazima yafuatwe, sababu tunaishi na jamii tofauti ambazo hatufanani nazo vizuri. Ukiacha hilo utengano wowote unapoteza uhalisia wa jamii nzima.

Mawazo yako ndiyo hukufanya
Uhuzunike.

Lord byron ni mwana falsafa na mshairi mahiri uingereza, aliwahi kusema kwamba “sanaa kubwa ya maisha ni maono, kuhisi mambo ni madogo hata katika maumivu” 
{The great art of life is sensation, to feel that weexist even in pain}
Tuchukulie usemi huu kama somo la kuwafundisha wale wanaolia kwa matatizo mbalimbali maishani. Katika maisha ya kila siku hayakosekani mambo ya kuumiza. 
Kuna kuugua, kufiwa, kukosa chakula, kusalitiwa penzini nk. Ni mambo ambayo huzaa huzuni na machozi miongoni mwa watu wengi.     
Lakini jambo la kujiuliza ni kwamba tunalia au kuhuzunika kwa sababu matatizo yetu ni makubwa au tumekosa ufahamu wa maisha.

Hebu tujiulize ni wangapi tunahuzunikia mishahara midogo tunayolipwa
Kazini kwetu? Je katika huzuni hizo tushawahi kujiuliza kwamba ni binadamu wangapi hawana kazi? Kama hao wapo sasa ukubwa wa tatizo la kukosa kazi unaotuliza kila siku uko wapi? Kimsingi uwiano wa shida na uhimili wake unaopatikana baina ya mtu na mtu  haubebi sifa ya huzuni kuletwa na tatizo kubwa, isipokuwa ni kukosekana kwa sanaa ya kuishi  kwa maono na hisia za kupunguza mambo makubwa kuwa madogo.

Katika hisia mwanadamu hawezi kuzuia machozi ya furaha au ya huzuni yasitoke.
Ifahamike kwamba kila mwanadamu ana uwezo wake wa kufanya zaidi ya tatizo analokutana nalo, lakini uwezo huo hauji kama sanaa ya maono na udogoshaji wa matatizo haujapewa kipaumbele. Kuna watu wanalia kila siku wanahitaji utajiri lakini hawafikii malengo kwa sababu wanaona umasikini ni jambo kubwa na kuufikia utajiri ni jambo kubwa pia.

Mtafiti mmoja aitwae William frey, anasema watu wanalia katika makundi sita tofauti ambayo ni: wenye kujawa na huzuni zinazosababishwa na matatizo 49% .
Wanaolia kwa furaha ni 21%. Wanaolia kwa hasira 10%. Wanaolia kwa huruma 7%. Huku wanaolia kwa wasiwasi ikiwa ni 5%. Wanaolia kwa hofu ni 4%.
Lakini pamoja na kuwepo kwa makundi hayo sita mwanadamu mwenyewe ana uwezo wa kuyabadili maono yake kwa kila kundi na kupata matokeo tofauti kabisa, kwani hasira ikipunguzwa kwa kuona kichocheo kilichojaza hasira hapo kidogo pumzi hushuka na mtu hujiona mwenye utulivu tofauti na mwanzo.

Vivyo hivyo kwa anayelia kwa huzuni, huruma, wasiwasi na hofu.
Kwa mantiki ileile hakuna haja ya kuhuzunika kwa kiwango cha juu wakati kuna kiwango cha chini cha kujiweka huru, nacho ni cha kutazama mambo makubwa kama madogo yasiyodumu na kwamba saa, siku, miaka michache ijayo
yatapita. Jiulize hapo ulipo kinakuliza kitu gani?
Fahamu kwamba hulii au kuhuzunika kwa sababu matatizo ni makubwa, bali umekosa ufahamu wa maono.

Hebu chukua jukumu la kudharau shida zako kwa kujilinganisha na wengine ambao bila shaka wanakuzidi. Fanya hivyo kila unapokabiliwa na tatizo, usilione tatizo ni kubwa kwa takwimu, lichukulie kuwa ni dogo kisha uanze kulishughulikia utaona linamalizika kwa ushindi mkubwa.
Kamwe usijaribu kulitatua tatizo ndani ya maono yanayolikuza kwani hutapata matokeo mazuri. Ukiwa ni umasikini uone ni mdogo, kufukuzwa kazi, kutokuzaa, kuteswa kwenye mapenzi na matatizo yote yatakayokukuta katika maisha yako yaone ni madogo kisha tumia nguvu zako zote kuyakabili hakika utashinda.

Lord byron aliigundua kanuni aliyoipa jina la Byronic hero, ambayo ilikuwa na misingi ya kuishi kwa maono na kupunguza ukubwa wa mambo kwa kutumia fikra. Wengi walipata mafanikio makubwa, kwahiyo jaribu kupunguza matatizo badala ya kuyakuza kwa kuona hayawezekani kutatuliwa, utaona unashinda matatizo yako kirahisi kabisa.
Kwani binadamu anatakiwa kuamini kwamba kitu kisichowezekana kama hakikuwa hivyo basi hakufikiria vya kutosha, kwani unapofikiria vitu kwa vitendo na kusema haitawezekana, hiyo ni dalili ya kuwezekana kwake lakini na akili yako inakuwa imefika mwisho wa kufikiri.   

Ili kufanya chochote, kuna nguvu zinazokuunganisha na unachokihitaji.
Ni kutokana na aina ya kufikiri, mazingira na hali ya kifedha ni kipimo tosha cha kujua ni nini unachowaza, kwani sisi ni matokeo ya tulichofikiri, na huwa tunaitengeneza dunia kutokana na mawazo yetu.
Hakuna njia nyingine ya kufanyia kazi umakini wetu zaidi ya hisia za akili ambazo ndio msingi wa kila kitu, ukiufuata msingi huu utakuwezesha kufanya maajabu katika maisha yako. Kwahiyo jifunze kuongea na ukimya wako.

                                                       SURA YA PILI: 
    Wewe ni zaidi ya mwili wako.
Wengi wetu huipa miili yetu nafasi kubwa huku sisi wenyewe tukifuata nyuma yake.
Tunapoongozwa na miili yetu inamaana kuwa tumetoka kwenye kufikiri vizuri na kuamia kwenye kufikiri vibaya.
Kwavile miili haina kawaida ya kutafakari wala kukagua hali halisi, huwa haikubali kurudi nyuma kwenye utashi wala kuzingatia kanuni za maumbile.
Kama tunajizatiti na kusema kuwa tunaweza kukaa bila kula wala kunywa chochote kwa siku kadhaa tunaweza. Tunaweza kwa sababu akili imetutuma kuwa tunaweza.
Tunaweza kufanya yote hayo kutokana na mawazo yetu ya kina.

Dr. Joseph Murphy, katika kitabu chake cha The power of subconscious mind, anasema: “Unaweza kuyapa maisha yako nguvu zaidi, uwezo zaidi, afya zaidi furaha na raha zaidi, kwa kujifunza namna ya kuwasiliana na kutumia nguvu iliyojificha kwenye mawazo yako ya kina” Huu ndiyo ukweli kila mmoja anaweza kuthibitisha hilo kwa kufanya.
Lakini kwa upande mwingine inaonesha ni namna gani binadamu anavyohangaika.
Kuhangaika huku hutufanya tuweze kupambana na wenzetu kusiko na mwanzo wala mwisho, katika kutafuta kile ambacho tunakiita utajiri, furaha au amani ya maisha.

Bilashaka tunajifunza kupambana na sio kutafuta njia nzuri ya maisha, kuishi kwa kujua kanuni ndiyo njia muafaka ya kuwezesha mambo yetu kwenda kama tunavyotaka.
Kwa maneno mengine tunaweza kusema kama tunataka kuondoka katika mtego huu na tupate utajiri, afya au furaha ya kweli, inatubidi tutumie falsafa tofauti.
Katika kufanikisha kile tulichokikusudia, itatubidi tufanye kwa vitendo yote tutakayoyapata kutokana na falsafa hii mpya. Kama tunataka kuishi maisha ya utajiri, afya na furaha, inabidi tufuate kanuni Fulani.  

Moja ya kanuni hizo ni kujua kwamba una uwezo usio na kikomo, na hivi sasa unatumia chini ya asilimia moja ya utajiri wako wa nguvu, akili na roho.
Badala ya kujisemea moyoni “siwezi” huna budi kujua kwamba ile nguvu ambayo inauongoza ulimwengu inakuongoza nawe pia.

Amini kwamba nguvu hii hupandisha uwezo wako kutoka asilimia moja unayoitumia sasa hadi kufikia juu zaidi.
Kanuni nyingine ni kuelewa kwamba ulimwengu huu umeumbwa kutoka kwenye furaha na siyo kwenye mateso. Ulimwengu asili yake ni furaha ya ajabu, chochote tukionacho duniani ni furaha ambayo imebadilishwa.
Kama utajifunza kuwaona binadamu, wanyama na vitu vingine vsivyo na uhai kama furaha kubwa katika umbo tofauti ni furaha ya ajabu ambayo imebadilishwa tu.
 
Pia ni muhimu kujua kwamba utajiri mkubwa kuliko wote ni utajiri wa binadamu, hivyo ni muhimu kujaribu kuuboresha utajiri huo.
Maranyingi tunapozungumzia utajiri wa mali ya nchi, huwa tunazungumzia utajiri wa mali ya asili kama vile dhahabu, almasi, mafuta na nk. ni muhimu, lakini kiukweli kinachoifanya nchi iwe tajiri ni utajiri wa watu. Watu wanapokuwa wameelimika ndipo wanapoweza kuzalisha zaidi.

Mtaji wa masikini ni elimu, huitaji kurithi mapesa mengi ili uwe tajiri, kwani wapo waliopata pesa huku wakiwa hawana elimu pesa zikapotea kiajabu tu.
Boresha kwanza ujuzi wako, jichimbue uujue uwezo wako wa asili, uendeleze uwezo wako na utaweza kufanikisha malengo yako.
Ni jambo la busara kujua kwamba utajiri ni wa kupita tu, jali kitu ambacho ni cha kudumu. Hakuna ubaya kusumbukia mahitaji yako muhimu ya kila siku ili uweze kuishi.
Lakini unapaswa kujua kwamba vitu vya duniani si vyako milele siku moja utatenganishwa na vitu hivyo vya duniani ukiwemo mwili wako.

Wakati unapambana kutafuta mahitaji ya dunia, usisahau kutafuta utajiri wa kiroho ambao ni wakudumu na hauharibiki wala kupotea.
kumbuka utajiri wa kiroho siyo wa dini, bali kuwakubali wengine kama walivyo.
Hivi sasa watu wapo kwenye mapambano makali ya kugombea utajiri wa dunia.
Ukishatambua kwamba dunia ina utajiri wa kumtosha kila mmoja, fanya jitihada ya kuwapunguzia wengine mizigo yao.
Wasaidie wengine kwa moyo wako wote na isiwe unawasaidia kwa lengo binafsi  la kujinufaisha mwenyewe.

Ukifanya hivyo utaona furaha ya kweli na kwenda hatua moja mbele kuelekea kwenye dunia ambayo kila mmoja wetu atakuwa tayari kugawana kwa usawa mali ya ulimwengu huu. Watu wengi tunapambana kwa sababu hatujui kwamba kwenye ulimwengu huu kila kitu kipo na hakuna haja ya mtu kupambana ili akipate[Hii haimaanishi ukae bila shughuli] Ni suala la kujua tu kwamba kuna kanuni Fulani ambazo mtu akizifuata anaweza kufanikiwa. Kanuni kuu kuliko zote ni ile ya kufikiri vizuri na kujipenda ili kuwapenda wengine, hapo utabaini njia nyingi za kumudu kufika utakapo maishani.
Ila ni hadi ujaribu ndipo utakaposhangazwa na matokeo yake, kusoma tu haitoshi.
Unatakiwa kuamini kwanza kwamba unaweza, kwani uwezo huwa unatoka nje ya mwili wako.

Nguvu katika  Imani

Kwanza kabisa jamii inapaswa kujua kwamba kuna nguvu nyingi hapa duniani kiasi kwamba hukanganya. Nguvu hizi zipo chini ya mamlaka ya binadamu kwa sababu nazo zinafuata kanuni za kimaumbile.
Ni pale tunapozipa nguvu hizi uwezo usio wake ndipo tunapoingia kwenye kuzifanya zituzidi au kutudhibiti na kututesa.
Moja ya njia za kuziheshimu na kuzijali nguvu hizi ni kuamini kwamba hazipo kwa ajili ya kuleta uharibifu kwa binadamu. Hata kuibuka kwa popobawa na vitu vingine vinavyofanana na hilo, havina maana kuwa matukio hayo yanaweza kutoa uhai wetu.
Bali tunaweza kutoa uhai wetu kwa kuogopa tu.

Karne hii haipendezi kuendelea kuamini kwamba nguvu yoyote tusioijua ina maana ya jini au uchawi. Hii ni sababu dunia imeingia mahali ambapo binadamu amekuwa akigundua haraka uwezo mkubwa alionao.
Sababu binadamu anazungukwa na nguvu nyingi ambazo hazijui zote, inabidi mtu akiri kwa ufahamu kuwepo kwa nguvu hizi.
Kukiri kwa ufahamu maana yake ni ile hali ya kukubali kuwepo kwa nguvu za kimawazo bila kuamini kuwa ndani yake kuna nguvu za uchawi, ulozi au jini vinavyoweza kutengenezwa na jamii Fulani kwa lengo la kumdhuru aliyekusudiwa.

Cha muhimu hapa ni kujua kuwa kila nguvu iliyomzunguka binadamu iko chini ya uwezo wa binadamu kama ataamua iwe hivyo, kinachotakiwa ni kujua tu namna nguvu hizi zinavyofanya kazi na yeye kuishi kwa kufuata kanuni za kimaumbile ambazo ni pamoja na kuwa na mitazamo na mawazo safi.
Njia rahisi ya kuishi kwa kufuata kanuni za kimaumbile ni ile ya binadamu kuwa na mawazo na mitazamo minyoofu. Hii ni mitazamo ambayo haimuumizi, kumvunja nguvu, kumkatisha tamaa au kumtia wasiwasi mhusika  na wengine wanaomzunguka.

Hakuna nguvu inayopotea bure, hata nguvu hasi hurudi kinyume na mtu akadhani amelogwa sababu maelezo ya kuhalalisha kupatwa kwake na nguvu hizo hasi yanaweza kukosekana. Nguvu hizi hasi zinaweza kutengeneza matukio na kubuni madude yenye maumbo wa majini na popobawa.
Kila mmoja wetu ana nguvu ndani yake ambazo ni kubwa sana.
Nguvu hizi kwa sehemu kubwa ziko kwenye mawazo yetu.
Namna tunavyojitazama, kujiamini kutafsiri matukio, kuwatazama wengine na mazingira, hufanya tofauti kubwa kati yetu.

Itakuwa ni kama ndoto kwetu kukumbana na jini, uchawi na vitu vinavyofanana na hivyo kama tutatumia nguvu hizi tulizonazo vizuri.
Tukijua kwamba tuna nguvu hizi ambazo hupaliliwa na kukuzwa na namna tunavyoweza kuishi kwa kufuata kanuni za kimaumbile, hatuwezi kudhuliwa wala kuogopeshwa na matukio yanayohusisha uchawi. Jamii inaweza kuishi bila kutengeneza dhana ya vitu vya ajabu ambavyo kwa akili ya kawaida tu haviwezi kuleta hofu.
Uchawi ni istilahi tu, haina maana yoyote yenye kushikika. Hii inamaana kwamba uchawi siyo kitu Fulani maalum, bali ni dhana pana lakini yenye kulenga uharibifu.

0 comments:

Post a Comment